Creation Science Information & Links!
Bwana Yesu Kristo · Matthieu 6
Lord Jesus Christ · Matthew 6

   "Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni.  Basi wewe utoapo sadaka, usipige panda mbele yako, kama wanafiki wafanyavyo katika masinagogi na njiani, ili watukuzwe na watu.  Amin, nawaambieni, Wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe utoapo sadaka, hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume;  sadaka yako iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.  Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao.  Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.  Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi.  Basi msifanane na hao; maana Baba yenu anajua mnayohitaji kabla ninyi hamjamwomba."   Matthieu 6:1-8

   "Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje,  Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.  Utupe leo riziki yetu.  Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.  Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina."   Matthieu 6:9-13

   "Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi.  Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.  Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao.  Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso;  ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.  Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba;  bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi;  kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako.  Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru.  Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo!  Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.  Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?  Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao?  Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja?  Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti  nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.  Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba?  Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini?  Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.  Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.  Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake."   Matthieu 6:14-34


Bwana Yesu Kristo · Matthew 6
http://www.creationism.org/kiswahili/salvJesusMatt6_sw.htm



Hoja kuu:  Kiswahili
www.creationism.org